SIDO TDC ZAWA CHACHU YA UANZISHAJI VIWANDA KWA WAJASIRIAMALI

Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo ( SIDO ) limeendelea  kujizolea sifa na umaarufu mkubwa kutokana na huduma zake kwa wajasiriamali na hususani vituo vyake vya kuendeleza teknolojia (TDC). Vituo hivi vimekuwa chachu ya uanzishaji viwanda vidogo kwa kuwa mashine mbalimbali za usindikaji na uchakataji malighafi mbalimbali zimekuwa zinazalishwa kupitia vituo hivi.

Tanzania imejaliwa kuwa na malighafi mbalimbali zinazotokana na  kilimo, ufugaji na uvuvi. Malighafi hizi zinahitaji kuongezea thamani ili bidhaa mbalimbali ziweze kuzalishwa. Uongezaji thamani malighafi hizi unahitaji teknolojia mbalimbali za uzalishaji. Hii ilipelekea SIDO kuanzisha vituo vya kuendeleza teknolojia vijulikanavyo kama TDC.

SIDO TDC zipo kwenye mikoa ya Kilimanjaro, Arusha, Mbeya, Kigoma, Iringa, Lindi na Shinyanga. Kupitia vituo hivi, teknolojia mbalimbali zimekuwa zinazalishwa kulingana na malighafi  zinazopatikana katika mikoa husika  na hivyo  kuongezwa  thamani. Hii imepelekea kuzalishwa kwa mashine kama mashine za kuchakata ngozi, kusaga karanga, kusaga mahindi, kusindika kahawa, kuchakata mihogo, kufyatua matofali, kukamua juisi, n.k

Wajasiriamali wameweza kufaidika na vituo hivi na hivyo:
 wajasiriamali wabunifu  wameweza kuboresha mashine zao kwa kushirikiana na vituo hivi ambavyo  vimekuwa pia vinatengeneza vipuri mbalimbali kwa ajili ya kutengenezea mashine.

  wajasiliamali  wanaozalisha mashine mbalimbali wamekuwa wanapewa ushauri wa kiufundi.

 Kutokana na  kasi ya mabadiliko ya sayansi na Teknolojia, SIDO imekuwa  inaagiza mashine kutoka nje ya nchi ili wajasiriamali wenye uhitaji waweze kununua kwa ajili ya kuongeza thamani malighafi zao.

 Vituo hivi vimekuwa vinawasaidia wahunzi katika  wanaboresha wa vifaa vyao  na hivyo kuwa chanzo cha upatikanaji vifaa vingi vinavyotokana na chuma kama vile majembe, mashoka, mapanga, n.k

 Vipuri mbalimbali vimekuwa vinachongwa kutoka kwenye vituo hivi vikiwepo pia vipuri vya magari, mashine nyingine nyingi n.k 

 Vituo hivi vimekuwa vinatengeneza mashine kulingana na mazao  yaliyoainishwa  kupitia program ya Bidhaa Moja Wilaya Moja (ODOP) na hivyo kurahisisha  utengenezaji wa mashine na uanzishwaji wa viwanda kwa kasi kupitia wilaya zote ziliyopo katika kila mkoa.