WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA AZINDUA BODI MPYA YA WAKURUGENZI WA SHIRIKA LA KUHUDUMIA VIWANDA VIDOGO (SIDO)

Hivi karibuni, Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara,  Mheshimiwa Dkt. Ashatu K. Kijaji akiwa ameongozana na Katibu Mkuu wa Wizara, Dkt. Hashil T. Abdallah, walizindua Bodi mpya ya Wakurugenzi - SIDO. Uzinduzi huu unakuja baada ya  Rais wa Jamhuri ya  Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kumteua  Mhand. Mussa A. Nyamsigwa,  kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya SIDO. 

Katika uzinduzi  huo, Mwenyekiti wa Bodi ya SIDO, Mhandisi. Mussa A. Nyamsigwa, alimpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan- Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kumuamini na  kumteua kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya SIDO.  Aliongeza kuwa, anajua umuhimu wa SIDO  na mwamko wananchi walionao katika kuendeleza viwanda vidogo nchini. Ili kusaidia katika kuinua uchumi wa nchi kupitia SIDO, aliahidi kuitumia nafasi yake kama Mwenyekiti katika  kushauri na  kuwasaidia wananchi wengi  kuanzisha na kuendeleza viwanda vidogo nchini. 

Mwenyekiti wa Bodi aliiomba Serikali kupitia Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara,  iendelee kuiimarisha SIDO kwa rasilimali watu, vitendea kazi n. k  ili Shirika lizidi kujizatiti na kufikia malengo  yake. Aliongeza kuwa, katika utendaji wake wa kazi na SIDO, atahakikisha mazingira ya utoaji wa huduma yameimarishwa na pia mahitaji halisi na thamani halisi ya kifedha zitakazotumika yanazingatiwa.  Mwenyekiti wa Bodi wa SIDO kwa kushirikiana na wajumbe wengine wa Bodi  walionyesha utayari wa kushirikiana na  Menejimenti ya SIDO bega kwa bega  ili kufanya utendaji wa Shirika usikwame.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa SIDO, Mhandisi Profesa Sylvester Mpanduji,  alipata fursa ya kuelezea kwa mapana  huduma  mbalimbali zinazotolewa na  SIDO katika  kuwawezesha  wajasiriamali nchini  kuanzisha  na kuendeleza viwanda vidogo na vya kati.  Alizitaja baadhi ya hizo zikiwemo  maendeleo ya  teknolojia na ufundi; mafunzo kwa wajasiriamali na huduma za ugani; masoko na uwekezaji pamoja na utoaji wa mikopo.  Huduma hizi hutolewa katika Mikoa yote ya Tanzania Bara kupitia  Ofisi zake za SIDO zilizopo katika kila mikoa.

Pamoja na mambo mengine, Mkurugenzi Mkuu wa SIDO alionyesha mipango  mikakati ya Shirika  ikiwemo:-
• Kuhawilisha Teknolojia kwa wingi kupitia vituo vyake vya uendelezaji teknolojia ( TDCs) na kuendelea kuviimarisha huku ikianzisha vituo vingine vipya.
• Kuongeza wigo wa huduma za SIDO Kwa wajasiriamali kwa kutoa mafunzo, ushauri na huduma za Ugani kupitia TEHAMA na uimalishaji wa vituo wa Mafunzo na Uzalishaji ( NTPC )
• Kuendeleza mitaa ya Viwanda ya SIDO kwa kuweka miundombinu wezeshi na kukamilisha kutengeneza mfumo unganishi wa TEHAMA kwa Shirika ili kurahisisha mawasiliano ya kidigitali  kwa ofisi zote za shirika.
• Kuimarisha mfuko wa kuendeleza wajasiriamali kifedha kupitia mfuko wake wa NEDF.
• Kutangaza huduma za Shirika na bidhaa mbalimbali zinazozalishwa na  wajasirimali.
• Kuongeza idadi ya watumishi, kutoa motisha na kuwapatia Mafunzo ili kuendana na mabadiliko ya Teknolojia na kuongeza ufanisi  kwa kuwapatia vitendea kazi ili kuhakikisha huduma zinawafikia walengwa kwa wakati.
• Kuimarisha ushirikiano na wadau/ mashirika ya kitaifa na kimataifa  kwa lengo la kuzidi kuimarisha huduma zetu na kulijengea  uwezo Shirika.